Jumatano, 3 Juni 2015

 



MWAKA 1993 nilifanikiwa kumuona Abbas Gulamali kwa mara ya kwanza uso kwa uso. Alikuwa mtaani kwetu, kwa ajili ya kufanya mazungumzo na baba yake mdogo  Edibly Lunyamila aitwaye Emmanuel Katamba.

Lengo lilikuwa ni kumalizia mazungumzo, kumsajili Lunyamila kutoka Shinyanga Shooting kwenda Yanga. Nikiwa na ‘masela’ wengine wa mtaani, tulijazana dirishani na kusikiliza nusu ya sehemu ya mazungumzo, kabla ya kushitukiwa na kutimuliwa, halafu mlinzi akakaa kulinda dirisha tusichungulie tena.
Lakini nina uhakika hata ukimuuliza Lunyamila leo atakuambia, Lunyamila alisajiliwa kwa kitita cha Sh milioni 1, hilo ndilo lilikuwa dau kutoka Shinyanga Shooting kwenda Yanga!
Wakati alipojiunga Yanga, kamwe hakuna mchezaji aliyekuwa akilipwa mshahara licha ya timu hiyo kuwa na nyota kadhaa kama Issa Athumani na Sanifu Lazzaro ‘Tingisha’.
Mwaka 1995, Lunyamila aliondoka Yanga na kujiunga Malindi kwa dau kubwa la Sh milioni 3.5 akiweka rekodi kwa kumzidi Nico Bambaga ambaye alisajiliwa kwa Sh milioni 3. Wote wakaanza kula mshahara wa Sh 15,000 kwa mwezi.

Mwishoni mwa mwaka, Lunyamila na Bambaga walirejea Yanga baada ya Malindi kuvurugika, Wazambia kama Mordon Malitoli wakarudi kwao. Lunyamila aliiendelea kuwa nyota, shujaa na mwisho mwaka 1998 aliisaidia Yanga kufuzu kucheza Klabu Bingwa Afrika hatua ya makundi baada ya kuifunga Coffee ya Ethiopia ambayo ilikuwa imeing’oa Al Ahly ya Misri.
Baada ya ushindi huo, Kampuni ya MIC Tanzania maarufu kama Buzz ikajitokeza kuidhamini Yanga chini ya uongozi wa Abbas Tarimba kama sijakosea. Ikaanza kuvaa Simu Poa, wachezaji wa Yanga wakapata neema na kwa mara ya kwanza wakaanza kulipwa mshahara wa Sh 60,000 kwa mwezi.
Kabla walikuwa wakilipwa fedha za mapato ya geti, timu ikishinda wanapata zaidi, sare angalau na wakifungwa wakati mwingine, hakuna kabisa.
Siku chache zilizopita nilipoandika kuhusiana na wachezaji wa sasa kudai fedha rundo za usajili na mshahara huku wakiwa hawajatoa msaada wowote kwa timu zao, wako waliolaumu sana, kwamba siwatetei wachezaji.
Kamwe sihitaji kuwa shujaa kwa kuwatetea wachezaji, au jabali la kuwapinga, lakini naendelea kusimamia kwenye haki kwao, pia klabu zao kwa kuwa wote ni wadau wanaoweza kuukuza mpira au kuumaliza kabisa.
Nataka uangalie vizuri, sasa ni miaka 10 imepita tangu Lunyamila aliporejea Yanga akiacha mshahara wa Sh 15,000 kwa mwezi kutoka Malindi. Miaka mitatu baadaye angalau akaanza kupata mshahara wa Sh 60,000 ambao wakati mwingine walilipwa baada ya miezi mitatu.
Ramadhani Singano wa mwaka 2015, anahitaji kulipwa Sh milioni 60 za usajili, mshahara Sh milioni 2, safi, ni mzalendo wacha afaidike, lakini tukirejea katika kazi yake, ameifanyia nini hasa Simba? Hajaipa hata nafasi ya kushiriki michuano ya kimataifa au ubingwa wa Nani Mtani Jembe unaweza kuwa mafanikio makubwa sana?
Nataka uangalie uwezo wa Lunyamila yule miaka 10 iliyopita, anzia kwa Singano, nenda kwa Simon Msuva, mchukue Mrisho Ngassa, halafu jiulize, tunapiga hatua mbele au tunarudi nyuma.
Ubora wa Lunyamila wa miaka 10 iliyopita, bado uko juu maradufu ya wachezaji wetu wengi nyota wa sasa. Chukua makinda na wakongwe, kwa huruma ya kizalendo, wote tunawapigia kelele walipwe vizuri tukiamini watafanya vizuri zaidi!
Saleh Ally anayesema ukweli anaweza kuonekana ni chenga tu, lakini ukweli utabaki palepale kuwa kama tunakuwa na Lunyamila bora miaka 10 iliyopita, halafu miaka 10 baadaye tunakuwa na rundo la wachezaji wasiofikia uwezo wake, tunafikiri tunaweza kupiga hatua?
Aliyekuwa hapewi mshahara alikuwa bora, hatari, tishio hakuna mfano. Hii pia unaweza kuiona hata ukiangalia makipa wa sasa, mabeki wa sasa na hata viungo wa sasa, jaribu kutafuta kiungo wa Tanzania mwenye kariba ya Issa Athumani Mgaya, Hamisi Gaga ‘Gagarino’, Method Mogella ‘Fundi’, tumia muda wako wa kutosha, halafu niambie kiungo unayemjua sasa mwenye uwezo huo.
Kama yupo utaniambia, kama hayupo nitakuuliza kwa nini na kuna sababu ipi sasa ya wachezaji wetu kulipwa mishahara mikubwa? Ni fasheni tu, au timu zinataka kuonyesha uwezo wa kifedha tu?
Okwi wa leo tunayemshangaa ni sawa na Lunyamila wa mwaka 2005 ambaye alikuwa anaelekea kumaliza soka lake.
Wachezaji wamewahi kujipima kwamba uwezo walionao wao sasa ni mdogo kuliko ule waliokuwa nao akina Said Mwamba ‘Kizota’ enzi zile?
Kuna tatizo kubwa, wachezaji wajipime, vizuri walipwe vizuri lakini nao lazima wajikague na kuangalia kiasi gani wanazilipa klabu zao, wamezipa mafanikio gani nyumbani na kimataifa. Si kulialia tu kama Ndorobo huku mkononi wana buku na wanataka mzigo wa Sh elfu 64.


Licha ya klabu za Simba na Yanga kuanza kufanya usajili wa nyota mbalimbali katika kikosi chao kwa ajili ya maandalizi ya msimu ujao, uongozi wa Klabu ya Azam umetamka wazi kuwa, hauna haraka yoyote ya kufanya usajili.

Kikosi hicho cha Azam kinachonolewa na Muingereza, Stewart Hall, mpaka sasa bado hakijaanza harakati za usajili ukilinganisha na timu za Simba na Yanga ambazo mpaka sasa tayari zimeshasajili wachezaji zaidi ya wane kila moja.

Msemaji wa kikosi hicho, Jaffar Idd Maganga, alisema kuwa licha za wapinzani wao Simba na Yanga kuanza harakati za usajili, wao hawana haraka na jambo hilo, badala yake wanajipanga ili kuweza kufanya usajili makini na kwenye nafasi ambazo zina mapengo.

“Sisi kwa upande wetu wala hatuna shida ya kufanya usajili wa haraka kama baadhi ya timu zilivyoanza jambo hilo, badala yake tunajipanga tu huku tukisubiri muda ufike ndiyo tuanze kufanya hivyo.

“Usajili wetu utajikita zaidi katika maelekezo ya ripoti ambayo iliachwa na kocha ambapo tutasajili kulingana na nafasi ambazo tumeona zinahitaji kuongezewa nguvu,” alisema Maganga.




Baada ya kufanikiwa kunasa nyota watatu, uongozi wa Klabu ya Mbeya City, umefunguka kuwa hautafanya mabadiliko makubwa katika kikosi chake na kwa sasa wanasaka nafasi moja pekee ya mchezaji ambaye anaweza kucheza nafasi zaidi ya moja uwanjani.

Mbeya City imefanikiwa kumnasa beki Haruna Shamte (JKT Ruvu), kiungo Joseph Mahundi (Coastal Union) na mshambuliaji Gideon Brown  kutoka Ndanda FC huku wachezaji wake wawili, Deus Kaseke na Peter Mwalyanzi wakitua Yanga na Simba.
Katibu wa timu hiyo, Emmanuel Kimbe, alisema kuwa kwa kiasi kikubwa kwa sasa nafasi zote zina wachezaji na wanasaka mchezaji ambaye anamudu nafasi zaidi ya moja.
Kimbe alisema kuwa, msimu ujao vijana watapewa nafasi katika kikosi chao, ndiyo maana hawasajili wachezaji wengi kutokana na kuwa na vijana wenye uwezo mkubwa.
“Tumeshawasajili wachezaji takriban watatu wa nafasi tofauti, kwa sasa tunaangalia nafasi kama moja na tunataka mchezaji mwenye uwezo mzuri na awe anamudu kucheza nafasi zaidi ya moja, yaani kiraka.
“Lengo ni kuboresha kikosi lakini bado tuna wachezaji wengi wazuri vijana ambao tunaamini kabisa watapambana kuhakikisha tunafanya vizuri msimu ujao, hao tumewaongeza siyo kwamba tuna upungufu mkubwa sana,” alisema Kimbe.

 


Aliyekuwa kiungo wa Azam FC, Amri Kiemba, amejiweka sokoni kwa kusema kuwa yupo tayari kutua katika timu yeyote hata kama ni Simba kutokana na mkataba wake kuisha.

Kiemba alipelekwa Azam FC kwa mkopo wa miezi sita akitokea Simba ambako mkataba wake umekwisha mwishoni mwa msimu uliopita, hivyo kumfanya kuwa mchezaji huru.
Kiemba alisema kuwa kwa upande wake yupo kikazi zaidi, hivyo iwapo timu yoyote itamtaka, atakwenda kuichezea kwa kuwa yeye ni mchezaji huru na hata kama timu yake ya zamani ya Simba itamfuata atakuwa tayari kurudi.
“Mimi sichagui timu ya kuichezea kwani hiyo ndiyo kazi yangu na nipo tayari kwenda kuichezea timu yoyote ile ilimradi kukubaliana tu.
“Mipango yangu kwa sasa bado na siwezi kusema timu gani hasa inanifaa kuichezea msimu ujao, ila yoyote ile itakayokuja hata kama ni Simba mimi nipo kikazi zaidi.
“Kwa sasa hakuna timu hata moja iliyonifuata kutaka kunisajili kwa kuwa walikuwa hawaelewi kama mkataba wangu umekwisha,” alisema Kiemba.

 



Kiungo mshambuliaji mpya wa Yanga, Deus Kaseke, aliyetokea timu ya Mbeya City ya jijini Mbeya, ametangaza vita kwa kiungo mwenzake, Simon Msuva au Haruna Niyonzima, kwa kusema kuwa atajipanga kuhakikisha anapangwa katika kikosi cha kwanza.

Kaseke amesema ni lazima aonyeshe uwezo wa juu kuliko Simon Msuva kwa kuwa anataka akiwa Yanga acheze namba 11.
Kaseke amesajiliwa na Yanga hivi karibuni ambapo amekuja kuziba pengo la Mrisho Ngassa aliyetimkia Afrika Kusini katika timu ya Free State.
 Kaseke amesema kuwa kati ya namba tatu anazocheza 10, 11 na 7, namba 11 pekee ndiyo ambayo anaona ataitendea haki iwapo kocha Hans Pluijm atampanga.

“Mimi nacheza nafasi tatu ambazo ni saba, 10 na 11, lakini namba 11 kwa upande wangu ndiyo ninaiona kuwa huru zaidi pindi ninapoicheza, hivyo ningependa kocha anipange namba hiyo na nitajituma kuhakikisha napata nafasi, najua kuna wengine wanaweza kucheza hapo lakini nikijituma najua nitapewa kipaumbele.
“Iwapo mwalimu atanipanga katika namba hiyo, nitakuwa vizuri zaidi kuliko hizi nyingine zilizobakia.

“Kuhusu ushindani wa namba, nimejipanga vyema hata kama kuna watu, nitajituma kadiri ya uwezo wangu kuweza kumshawishi kocha,” alisema Kaseke.

Hakuna maoni: